Kumlinda Mtoto Dhidi ya Ajali Barabarani
Kumlinda Mtoto Dhidi ya Ajali Barabarani

Watoto wadogo huhitaji msaada kutoka kwa watu wakubwa pindi wakiwa kwenye mazingira ya barabara. Pia ni fursa kwao kujifunza kwa vitendo kuhusu mazingira na mienendo ya barabarani wakiwa na wakubwa wao, wazazi au walezi.Watoto wadogo hujifunza mienendo ya barabarani kwa kuangalia na kufanya au kuigiza kama watu wengine wafanyavyo. Kwahiyo kuwa mfano mwema kwao.Ongea na mwanao kuhusu barabara, alama, vyombo vya barabarani (mfano magari na pikipiki), namna na wapi pa kuvuka barabara kwa usalama.


Kwenye miaka ya mwanzo, watoto huhitaji msaada mkubwa kutoka kwa wakubwa zao ili kuweza kukabiliana na hali ya barabarani kiujumla. Wanahitaji msaada kutambua uwepo wa vyombo vya barabarani na madhara yanayo weza kusababishwa na vyombo hivyo. Vile vile  kuweza kutambua au kutabiri mwendo kasi na umbali wa magari yanayokuja. Wakiwa wanakua na kuendelea kupata mafunzo au maelekezo na ujuzi kutoka kwa jamii inayowazunguka, huwa na uelewa na wanaweza kusimama kwa ajili ya usalama wao wenyewe wakiwa barabarani na kuwa watumia barabara wanaofuata taratibu na kanuni za barabara.


Ni vizuri mtoto kupata ujuzi kuhusu usalama barabarani akiwa kwenye mazingira ya barabarani. Watoto hujifunza mambo mengi kwa kuona na kupitia uzoefu. Muingiliano wa watoto na wakubwa huwasaidia kujifunza mengi kuhusu barabara na usalama barabarani. Unaweza kuongea  na mtoto wako mkiwa manatembea, muulize  maswali kuhusu barabara, alama, magari, pikipiki n.k. Na namna gani na wapi anaweza ukavuka barabara kwa usalama.


Lengo la makala hii ni kukufunza namna ya kumsaidia mtoto kuwa salama akiwa barabarani ikiwemo usalama barabarani kwa watoto chini ya miaka mitano, watoto kati ya miaka mitano na tisa na watoto kati ya miaka 10 mpaka 15.

 

Uslama barabarani kwa watoto chini ya miaka mitano

Muda wote waelekeze watoto kwa umakini kuhusu hali ya barabarani na ni muhimu kufanya yafuatayo:-

Ø Ongea na mwanao kuhusu mazingira ya barabarani;

Ø Mwanao akianza kutembea na wewe mwambie kwamba wakati wote ashikwe mkono na wakubwa anaowafahamu pindi akiwa barabarani na kutembea pembeni mwa barabara upande wa kulia au kwenye njia ya waenda kwa miguu. Ongea na mwanao ni kwanini na kuna umuhimu gani kushikwa mkono akiwa barabarani;

Ø Mwelezee kitendo au matendo yanayofanyika wakati mnavuka barabara pamoja. Mhusishe mwanao kwenye kufanya maamzi kuhusu wakati salama wa kuvuka barabara, pamoja na hili bado atakaye fanya maamzi ya kuvuka barabara ni wewe ila kwa kitendo hicho utakuwa unampa mtoto uwezo wa kufikiri kwenye mazingira ya barabarani;

Ø Muda wote kuwa mfano mzuri kwa mwanao kwa kuvaa mkanda wa usalama, kutii sheria na kanuni za barabarani, kuendesha kwa ufanisi na utaratibu uliowekwa ukiwa barabarani;

Ø Angaliana na watumiaji wengine wa barabara sana sana kwenye makutano ya barabara;

Ø Mhusishe mwanao kwenye kuchagua maeneo salama ya kucheza;

Ø Vile vile mwelezee mwanao tofauti kati ya  njia ya waenda kwa miguu na barabara,  namna ya kutembea na mkubwa wanayemfahamu na kushikana mikono pindi wakiwa karibu na barabara au barabarani, mueleweshe maana ya simama, angalia, sikiliza na fikiri kwa vitendo, mwelezee ni maeneo gani salama ya kuvuka barabara na kuwa mwangavu ili kuonekana na watumiaji wengine wa barabara.

 

Usalama barabarani kwa watoto kati ya miaka mitano hadi tisa

Mtoto wako bado anahitaji uangalizi na msaada akiwa kwenye mazingira ya barabarani, hivyo fanya yafuatayo:-

Ø Ongea na mwanao kuhusu alama za barabarani na taa za barabarani, onesha na mwelezee maeneo salama ya kuvuka barabara;

Ø Mfundishe mwanao namna ya kuvuka barabara kwa kutumia ‘simama, angalia, sikiliza na fikiri au tafakari’ ambapo atasimama kando ya barabara, ataangalia na kusikiliza mtiririko wa magari na ataamua kama ni salama kuvuka ama la. Panga safari nenda naye shuleni, pita njia salama ya kwenda kwa miguu, na tumia sehemu salama kuvuka barabara kama vile vivuko vya waenda kwa miguu na sehemu za barabara zilizo nyooka;

Ø Mwelekeze mwanao njia nzuri na salama za kwenda na kurudi kutoka shuleni;

Ø Muda wote kuwa mfano mzuri, kwa mwanao kwa kuvaa mkanda wa usalama, kufuata sheria na taratibu za barabarani na undeshaji wa kujihami.

Ø Uliza shuleni kwa mwanao kuhusu miradi au mafunzo yanayoendeshwa shuleni hapo kuhusu usalama baabarani kwa ajili ya wanafunzi.

 

Usalama barabarani kwa watoto kati ya miaka  kumi hadi kumi na tano

Watoto kati ya miaka 10 na 15 wanaweza kumudu mazingira ya barabarani. Ila hii itategemea na kiasi cha uelewa au uzoefu wa mtoto huyo alicho nacho kuhusu mazingira ya barabarani. Nafasi  ya mwanao kuumia akiwa barabarani kwenye umri huu ni kubwa kuliko watoto wadogo, misukumo ya vijana wenzake inaweza kupelekea tabia hatarishi wakiwa barabarani. Kundi hili linakuwa na uwezekano mkubwa wa kupata ajali likiwa barabarani sababu ya safari ndefu kutoka mashuleni wakiwa wenyewe na marafiki zao. Hivyo ni  muhimu kuzingatia yafuatayo:-

Ø Hakikisha mwanao anaelewa umuhimu wa kutembea moja kwa moja kuelekea nyumbani na sio vinginevyo;

Ø Hata kama mwanao amefikia umri wa balehe endelea kuongea nae kuhusu usalama barabarani, na hakikisha anafahamu na kuendelea kuchukua tahadhari pindi akiwa barabarani;

Ø Fuatilia na angalia kama mwanao muda wote husimama, huangalia, husikiliza na kutafakari au kufikiri wakati akivuka barabara. Muulize akuelezee nini anafanya na kwa nini anafanya hivyo akiwa barabarani;

Ø Ongea na mwanao kuhusu sheria za barabarani. Nenda nae ukiwa unaendesha gari kama itawezekana na tembea nae barabarani;

Ø Panga na mwanao kuhusu njia salama kuelekea shuleni na maeneo ambayo mwanao hutembelea mara kwa mara;

Ø Hakikisha mwanao anavaa nguo angavu ambazo zitaonekana kirahisi na watumiaji wengine wa barabara.   

Shirika La Elimu ya Utekelezaji wa Sheria