Matumizi ya Taa za Barabarani
Matumizi ya Taa za Barabarani

Taa za barabarani ni moja ya ishara za usalama barabarani na zipo kwa mujibu wa sheria ya usalama bararani sura ya 168 ya mwaka 2002.  Taa za barabarani maranyingi hufungwa pembeni, au katikati ya barabara kwa lengo la kuongoza mserereko wa magari barabarani pamoja na kuweka uwiano sawa wa matumizi ya njia kwa makundi yote ya watumia barabara, kama wenye vyombo vya moto, waenda kwa miguu, waendesha baiskeli, wasukuma mikokoteni. Kwa mujibu wa sheria ya usalama barabarani ya mwaka 2002 sura ya 168 kifungu No. 73(2) watumiaji wote wa barabara wanatakiwa kuheshimu na kufuata ishara zinazooneshwa na taa za barabrani.

 

Aina za Taa za Barabarani

Nyekundu

Taa nyekundu barabarani huonesha ishara ya SIMAMA. Vyombo vya moto nyote barabarani vinalazimika kusimama pale rangi ya taa zinazoongoza vyombo hivyo pamoja na watumiaji wengine wa barabara kuonesha rangi nyekundu. Kwa mujibu wa sheria ya usalama barabarani ni kosa kisheria kuvuka taa nyekundu. Mbali na kuwa ni kosa pia ni hatari kutumia barabara kwa wakati huo kwasababu unaweza kusababisha ajali. Hii ni kutokana na kuwa ishara inayoonekana na taarifa inayotolewa kwa wakati huo ni kuwa siyo zamu yako kutumia barabara kwa wakati huo bali ni zamu ya watumiaji wengine. Wanaweza kuwa waenda kwa miguu au ni wakati wa U-turn au makutano ya barabara. Katika mazingira hayo ni rahisi ajali kutokea.

 

Kwa vivuko vya waenda kwa miguu vinavyoongozwa na taa, waenda kwa miguu pia  wanalazimika kusimama pale mtu wa rangi nyekundu anapooneshwa kwenye taa. Lakini pale ambapo mwenda kwa miguu anataka kukatiza bararaba na sehemu hiyo haina alama ya punda milia, anatakiwa kukatiza barabara pale ambapo taa inaonesha rangi nyekundu na magari yote yamesimama kutoka pande zote. Wakati wa kuvuka ni lazima atumie kanuni za uvukaji salama wa barabara.

 

Mshale mwekundu pia unakuwa na maana ile ile kuwa unatakiwa kusimama hadi pale mshale wa kijani utakapoonekana.

 

Njano

Taa ya njano hutoa ishara ya “TAHADHARI” na “JITAYARISHE KUSIMAMA”. Maana ya taa hii ni kuwa jitayarishe kusimama kwasababu taa nyekundu ipo karibu kuwaka. Ni wajibu wa dereva kusimama anapoona taa ya njano iwapo ni salama kufanya hiyo, yaani unauwezo wa kusimama bila kusababaisha usumbufu au hatari yoyote barabarani kwa wakati huo. Lakini endapo umekwisha ikaribia taa na kwa wakati huo ameona kuwa siyo salama kusimama basi sheria inakuruhusu kupita.

Mshale wa njano unamaana ya kuwa punguza mwendo na simama mshale mwekundu upo karibu kuwaka.

 

Kijani

Taa hii inamaana ya NENDA. Lakini kabla ya kuondoka ni wajibu wako kuhakikisha wanaovuka na kutumia barabara kwa wakati huo wamepita. Mfano kwenye makutano ya barabara au kwenye U-turn magari yote yamepita barabarani. Kwenye vivuko vya waenda kwa miguu vinavyoongozwa na taa, wanapotaka kukatiza barabara ni sharti wasubiri mpaka mtu wa rangi ya kijani anapoonekana kwenye taa.

Mshale wa kijani una maana ileile ya kupita uelekeo ule tu ambao unaoneshwa kwenye mshale, inaweza kuwa kushoto ama kulia. Angalizo ni kuwa kabla hujapinda kulia au kushoto sawasawa na mshale unavyokuongoza ni lazima uhakikishe kuwa magari na watumiaji wengine wa barabara wamesimama na hawapo barabarani kwa wakati huo.

Kwa mujibu wa sheria ya usalama barabarani ya mwamka 2002 sura ya 168 kifungu cha 73(4)  sehemu ambazo kuna taa, michoro na ishara za usalma barabarani lakini pia kuna askari wa usalama barabarani, sheria inasema kuwa kwa wakati huo ishara na maelekezo ya askari wa usalama barabarani ndiyo yanatakiwa kufuatwa nakupewa kipaumbele.

 

NB

Endapo taa za barabarani zimezima kwa wakati huo kutokana na tatizo la kiufundi au umeme kukata watumiaji wote wa barabara wanaaswa kutumia njia kwa zamu. Ni lazima kusimama unapokaribia makutano ya barabara ili kutoa nafasi kwa wanaotumia njia kwa wakati huo na zamu yao inapoisha basi ni zamu yako kutumia njia kwa wakati huo. Ni lazima pia kutumia njia kwa uangalifu mkubwa maeneo ya makutano ya barabara na endapo taa za barabarani zimezima na hakuna askari au mtu mwenye mamlaka kisheria kuongoza magari.

PESACO TANZANIA